Exodus 10

Pigo La Nane: Nzige

1 aNdipo Bwana akamwambia Musa, “Nenda kwa Farao, kwa kuwa nimeufanya moyo wake kuwa mgumu na mioyo ya maafisa wake ili kwamba nipate kutenda ishara hizi zangu za ajabu miongoni mwao 2 bili upate kuwaeleza watoto wako na wajukuu wako jinsi nilivyowatendea Wamisri kwa ukali na jinsi nilivyofanya ishara zangu miongoni mwao, nanyi mpate kujua kuwa Mimi ndimi Bwana.”

3 cKwa hiyo Musa na Haruni wakaenda kwa Farao na kumwambia, “Hili ndilo Bwana, Mungu wa Waebrania, asemalo: ‘Utaendelea hata lini kukataa kunyenyekea mbele yangu? Waachie watu wangu waende, ili wapate kuniabudu. 4 dKama ukikataa kuwaachia waende, kesho nitaleta nzige katika nchi yako. 5 eNao watafunika uso wa ardhi hata usionekane. Watatafuna mabaki machache yaliyobakizwa baada ya ile mvua ya mawe, yaani pamoja na kila mti unaoota katika mashamba yenu. 6 fNzige hao watajaza nyumba zako, za maafisa wako wote na za Wamisri wote. Jambo ambalo baba zenu wala babu zenu hawajapata kuona tangu siku ile walipoanza kuishi katika nchi hii mpaka leo hii.’ ” Ndipo Musa akageuka na kumwacha Farao.

7 gMaafisa wa Farao wakamwambia, “Mpaka lini huyu mtu atakuwa tanzi kwetu? Waachie hao watu waende zao, ili wapate kumwabudu Bwana Mwenyezi Mungu wao. Je, bado hutambui kuwa Misri imeangamia?”

8 hNdipo Musa na Haruni wakaletwa kwa Farao. Farao akawaambia, “Nendeni, mkamwabudu Bwana Mwenyezi Mungu wenu. Lakini ni nani hasa watakaokwenda?”

9 iMusa akajibu, “Tutakwenda na vijana wetu na wazee, pamoja na wana wetu na binti zetu, pia pamoja na kondoo zetu, ng’ombe, mbuzi, farasi na punda kwa sababu tutaadhimisha sikukuu kwa Bwana.”

10Farao akasema, “Bwana awe pamoja nanyi, kama nikiwaruhusu mwondoke pamoja na wanawake wenu na watoto wenu! Ni wazi kwamba mna makusudi mabaya. 11La hasha! Wanaume peke yao na waende, wakamwabudu Bwana, kwa kuwa hilo ndilo mmekuwa mkiomba.” Kwa hiyo Musa na Haruni wakaondolewa mbele ya Farao.

12 jBasi Bwana akamwambia Musa, “Nyoosha mkono wako juu ya Misri ili kundi la nzige liweze kuingia juu ya nchi na kutafuna kila kitu kiotacho katika mashamba na kila kitu kilichosazwa na ile mvua ya mawe.”

13 kKwa hiyo Musa akanyoosha fimbo yake juu ya Misri, Bwana akauleta upepo wa mashariki ukavuma katika nchi yote mchana wote na usiku kucha, kufikia asubuhi upepo ukawa umeleta nzige. 14 lWakaivamia Misri yote na kukaa kila eneo la nchi kwa wingi. Kamwe hapajapata kuwepo pigo la nzige kama hilo, wala halitakuwepo tena. 15 mWakafunika ardhi yote mpaka ardhi ikawa nyeusi. Wakatafuna kile chote kilichokuwa kimebakizwa na ile mvua ya mawe, kila kitu kiotacho mashambani pamoja na matunda kwenye miti. Hakuna kitu chochote cha kijani kilichosalia katika miti au mmea katika nchi yote ya Misri.

16 nFarao akawaita Musa na Haruni kwa haraka na kuwaambia, “Nimetenda dhambi dhidi ya Bwana Mwenyezi Mungu wenu na dhidi yenu pia. 17 oSasa unisamehe dhambi yangu mara moja tena na umwombe Bwana Mwenyezi Mungu wako aondoe pigo hili baya kwangu.”

18 pKisha Musa akaondoka kwa Farao akamwomba Bwana. 19Naye Bwana akaugeuza upepo ukavuma kutoka magharibi, wenye nguvu nyingi, ambao uliwaondoa wale nzige na kuwapeleka kwenye Bahari ya Shamu. Hakuna nzige hata mmoja aliyebaki popote katika nchi ya Misri. 20 qLakini Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, wala hakuwaachia Waisraeli waondoke.

Pigo La Tisa: Giza

21 rKisha Bwana akamwambia Musa, “Nyoosha mkono wako kuelekea angani ili giza litande katika nchi ya Misri, giza ambalo watu wanaweza kulipapasa na kulihisi.” 22 sKwa hiyo Musa akaunyoosha mkono wake kuelekea angani, na giza nene likafunika pote katika nchi ya Misri kwa muda wa siku tatu. 23 tHakuna mtu yeyote aliyeweza kumwona mwenzake, wala kuondoka mahali alipokuwa kwa muda wa siku tatu. Lakini Waisraeli wote walikuwa na mwanga katika maeneo yao waliyokuwa wanaishi.

24 uNdipo Farao akamwita Musa na kusema, “Nendeni, mkamwabudu Bwana. Hata wanawake na watoto wenu mwaweza kwenda nao pia, lakini kondoo, mbuzi na ng’ombe wenu waacheni.”

25 vLakini Musa akasema, “Huna budi kuturuhusu tuwe na dhabihu na sadaka za kuteketezwa za kutoa mbele za Bwana Mwenyezi Mungu wetu. 26Sisi ni lazima tuondoke na mifugo yetu pia, wala hakuna ukwato utakaoachwa nyuma. Inatupasa kutumia baadhi ya hiyo mifugo katika kumwabudu Bwana Mwenyezi Mungu wetu, kwa kuwa mpaka tutakapofika huko hatutakuwa tumefahamu ni nini tutakachotumia katika kumwabudu Bwana.”

27 wLakini Bwana akaufanya moyo wa Farao kuwa mgumu, hakuwa radhi kuwaachia waondoke. 28Farao akamwambia Musa, “Ondoka mbele yangu! Hakikisha kuwa hutakuja mbele yangu tena! Siku ile utakapouona uso wangu utakufa.”

29 xMusa akamjibu, “Iwe kama ulivyosema! Kamwe sitauona uso wako tena.”
Copyright information for SwhKC